Ofisi ya Rais
Maendeleo ya Vijana
VIJANA WAMETAKIWA KULINDA AMANI NA UMOJA WA KITAIF...

VIJANA WAMETAKIWA KULINDA AMANI NA UMOJA WA KITAIFA KWA MAENDELEO YA NCHI

13 Apr, 2026
VIJANA WAMETAKIWA KULINDA AMANI NA UMOJA WA KITAIFA KWA MAENDELEO YA NCHI

Mkuu wa Wilaya ya Ubungo, Mhe. Albert Gasper Msando ameongoza uzinduzi wa Jukwaa la Vijana “Vijana Platform” katika Halmashauri ya Manispaa ya Ubungo, tukio ambalo limefanyika katika ukumbi wa The Little Flower, Goba.

Mhe. Msando amesema kwamba serikali inaendelea kuchukua hatua mathubuti kuwezesha vijana kiuchumi, ikiwemo kuunda majukwaa ya uwezeshaji vijana kiuchumi pamoja na kuwapa mikopo ya kuwawezesha kujiajiri, hivyo amewataka vijana kuwa tayari kutumia fursa zinazotolewa na serikali.

Vilevile, amewataka vijana kuheshimu sheria za nchi ikiwemo kutumia mitandao ya kijamiii kwa usahihi na kuepuka kutengeneza na kusambaza taarifa potofu zinazoleta taharuki, na kuondoa utulivu katika jamii.

“Tuna mambo mengi sana kwenye mitandao ya kijamii, tuna fursa nyingi sana huko lakini mara nyingi tunashindwa kung’amua mambo yanayotufaa.” Mhe. Msando Amesema.

Uzinduzi wa Vijana Platform umeenda sambamba na vijana kufundishwa elimu ya uraia na uzalendo, kupitia mada ambayo imewasilishwa na Kate Sylvia Magdalena Kamba ambaye amesisitiza vijana kujenga mshikamano na umoja wa kitaifa, na kulinda amani.

Kwa upande wake, Dkt. Damian Shumbusho amewaasa vijana kutambua nafasi yao katika jamii ili kujenga taifa la watu wenye upendo, umoja na kuheshimu utawala wa sheria.

Dkt. Shumbusho amesema kwamba ili taifa lolote liweze kuendela linategemea vijana wake ambao ndio nguvu kazi kuwa wabunifu, wanaojituma, na wenye uzalendo na malengo ya kuendeleza taifa lao.

Pamoja na mambo mengine, vijana wamefundishwa pia kuhusu kuibua fursa za kiuchumi kulingana na mazingira yanayowazunguka, uadilifu na uwajibikaji.